1Wakumbushe watu kuwastahi watawala na wenye mamlaka, kuwatii na kuwa tayari kwa kila namna kutenda mambo yote mema. 2Waambie wasimtukane mtu yeyote; bali waishi kwa amani na masikizano, wawe daima wapole kwa kila mtu. 3Maana, wakati mmoja sisi tulikuwa wapumbavu, wakaidi na wapotovu. Tulikuwa watumwa wa tamaa na anasa za kila aina. Tuliishi maisha ya uovu na wivu; watu walituchukia nasi tukawachukia. 4Lakini wakati wema na upendo wa Mungu, Mwokozi wetu, ulipofunuliwa, 5alituokoa. alituokoa si kwa sababu ya jambo lolote jema tulilotenda sisi, bali alituokoa kwa sababu ya huruma yake, kwa njia ya Roho Mtakatifu anayetujalia tuzaliwe upya na kuwa na maisha mapya kwa kutuosha kwa maji. 6Mungu alitumiminia Roho Mtakatifu bila kipimo kwa njia ya Yesu Kristo, Mwokozi wetu, 7ili kwa neema yake tupate kukubaliwa kuwa waadilifu na kuupokea uzima wa milele tunaoutumainia. 8Jambo hili ni kweli. Ninakutaka uyatilie mkazo mambo haya, ili wale wanaomwamini Mungu, wawe na hamu ya kuutumia wakati wao katika kutenda mema, ambayo ni mambo mazuri na ya manufaa kwa watu. 9Lakini jiepushe na ubishi wa kipumbavu, ugomvi na mabishano juu ya Sheria. Mambo hayo hayana faida yoyote na ni ya bure tu. 10Mtu anayesababisha mafarakano mpe onyo la kwanza na la pili, kisha achana naye. 11Wajua kwamba mtu wa namna hiyo amepotoka kabisa, na dhambi zake zathibitisha kwamba amekosea. 12Baada ya kumtuma kwako Artema au Tukiko, fanya bidii kuja Nikopoli unione, maana nimeamua kukaa huko wakati wa majira ya baridi. 13Jitahidi kumsaidia mwana sheria Zena na Apolo ili waweze kuanza ziara zao na uhakikishe kwamba wana kila kitu wanachohitaji. 14Ni lazima watu wetu wajifunze kuutumia wakati wao katika kutenda mema ili wasaidie katika mahitaji ya kweli, na maisha yao yawe ya kufaa. 15Watu wote walio pamoja nami wanakusalimu. Wasalimu rafiki zetu katika imani. Nawatakieni nyote neema ya Mungu.