1Kwa hiyo, ndugu zangu, maadam Mungu ni mwenye huruma nyingi, nawasihi kwa moyo wote: jitoleeni nafsi zenu kwa Mungu kama tambiko iliyo hai, takatifu na yenye kupendeza. Hii ndiyo njia yenu halisi ya kumwabudu. 2Msiige mitindo ya ulimwengu huu, bali Mungu afanye mabadiliko ndani yenu kwa kuzigeuza fikira zenu. Hapo ndipo mtakapoweza kuyajua mapenzi ya Mungu, kutambua jambo lililo jema, linalompendeza na kamilifu. 3Kutokana na neema aliyonijalia Mungu, nawaambieni ninyi nyote: msijione kuwa ni kitu zaidi kuliko mnavyopaswa kuwa. Fikira zenu na ziwe na kiasi kufuatana na kipimo cha imani Mungu aliyomgawia kila mmoja. 4Mwili una viungo vingi, kila kimoja na kazi yake. 5Hali kadhalika ingawa sisi ni wengi, tu mwili mmoja kwa kuungana na Kristo, na kila mmoja ni kiungo cha mwenzake. 6Basi, tunavyo vipaji mbalimbali kufuatana na neema tuliyopewa. Mwenye kipaji cha unabii na akitumie kadiri ya imani yake. 7Mwenye kipaji cha utumishi na atumikie. mwenye kipaji cha kufundisha na afundishe. 8Mwenye kipaji cha kuwafariji wengine na afanye hivyo. Mwenye kumgawia mwenzake alicho nacho na afanye hivyo kwa ukarimu. Msimamizi na asimamie kwa bidii; naye mwenye kutenda jambo la huruma na afanye hivyo kwa furaha. 9Mapendo yenu na yawe bila unafiki wowote. Chukieni jambo lolote ovu, zingatieni jema. 10Pendaneni kidugu; kila mmoja amfikirie mwenzake kwanza kwa heshima. 11Msilegee katika bidii, muwe wachangamfu rohoni katika kumtumikia Bwana. 12Tumaini lenu liwaweke daima wenye furaha; muwe na saburi katika shida na kusali daima. 13Wasaidieni watu wa Mungu katika mahitaji yao; wapokeeni wageni kwa ukarimu. 14Watakieni baraka wote wanaowadhulumu ninyi; naam, watakieni baraka na wala msiwalaani. 15Furahini pamoja na wanaofurahi, lieni pamoja na wanaolia. 16Muwe na wema uleule kwa kila mtu. Msijitakie makuu, bali jishugulisheni na watu wadogo. Msijione kuwa wenye hekima sana. 17Msilipe ovu kwa ovu. Zingatieni mambo mema mbele ya wote. 18Kadiri inavyowezekana kwa upande wenu, muwe na amani na watu wote. 19Wapenzi wangu, msilipize kisasi, bali mwachieni Mungu jambo hilo; maana Maandiko Matakatifu yasema: “Kulipiza kisasi ni shauri langu; mimi nitalipiza asema Bwana.” 20Tena, Maandiko yasema: “Adui yako akiwa na njaa, mpe chakula; akiwa na kiu, mpe kinywaji. Maana kwa kufanya hivyo utamfanya apate aibu kali kama makaa ya moto juu ya kichwa chake.” 21Usikubali kushindwa na ubaya, bali ushinde ubaya kwa wema.